Jumamosi, 24 Januari 2015

Tehama shuleni; Dhamira njema iliyokosa mikakati wezeshi

Kwa ufupi. Pamoja na dhamira njema ya Serikali kutaka Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kutumika, mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji, imeshindwa kuandaa mazingira ya kuwezesha teknolojia hiyo kufanya kazi katika shule za msingi na sekondari hasa zile za umma.

Soma kisa hiki; Mgeni anakuja nchini na kutaka pamoja na mambo mengine kuwafundisha kompyuta watu wa jamii ya wafugaji ambao asili yao ni maisha ya kuhamahama porini.
Mkutano unaitishwa na mkataba wa makubaliano unawekwa kati yake na watendaji wa Serikali ili atoe elimu hiyo vijijini. Baada ya mkutano sote tunashangilia.
Hadithi hii inashabihiana na yanayotokea sasa katika sekta ya elimu nchini. Ilivyo ni kuwa baadhi ya mipango ya kielimu haina tija kwa kuwa haitekelezeki, japo dhamira yake ni nzuri.
Kama haitoshi mipango hiyo siyo kipaumbele muhimu kwa jamii licha ya ukweli kuwa imekuwa ikianzishwa kwa mbwembwe na ahadi lukuki.
Tehama shuleni
Kilele cha maono duni ya wale waliopewa jukumu la kusimamia elimu yetu, linajionyesha katika mipango iliyopo ya kutaka zana za kisasa za Tehama zitumike katika kufundishia na kujifunzia shuleni.
Mfano mzuri ni mpango wa hivi karibuni ambapo , Serikali kwa kushirikiana na kampuni za Vodacom na Samsung wameanzisha mpango wa kuziunganisha shule za sekondari nchini na mkongo wa mawasiliano wa taifa.
Hatua hiyo itatoa fursa kwa shule kutumia kompyuta zilizounganishwa na intaneti katika kufundishia na kujifunzia.
Hata hivyo, pamoja na dhamira hii njema, swali la msingi ni je, shule hizo zina miundombinu tayari kwa kuunganishwa na mkongo wa mawasiliano?
Kinachoshangaza ni kuwa mipango yote hii inabuniwa ilhali hakuna mikakati ya kuweka mazingira wezeshi shuleni, kama vile uwepo wa nishati ya umeme ambayo ni muhimu katika matumizi ya Tehama.
Kwa mujibu wa Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa, hadi mwaka 2012 shule mbili za msingi na tano za sekondari (wasioona) ndizo zilizokuwa zimenufaika na mradi huo wa mawasiliano ya mkongo wa taifa kati ya maelfu ya shule zilizopo nchini.
Kwa mujibu wa Profesa Mbarawa shule za msingi zilizonufaika ni Buigiri (Dodoma) na Kizega (Singida). Shule za sekondari zilizonufaika mpango huo ni Ilula (Iringa), Mpwapwa (Dodoma), Ilowola (Njombe), Tumaini na Lulumba (Singida).



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni